Mwigulu “Sekta binafsi ikinawiri na Serikali inanawiri“

 

WAZIRI wa Fedha na Mipango Dk. Mwigulu Nchemba amekihakikishia Chama cha Watoa Huduma za Simu Tanzania (TAMNOA) kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri ya biashara yatakayo iwezesha Sekta Binafsi kukua na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Nchemba alisema hayo jijini Dodoma alipokutana na kuzungumza na Chama cha Watoa Huduma wa Simu Tanzania (TAMNOA), wakati kikiwasilisha Serikalini maoni yao kuhusu sera za kodi ikiwa ni maandalizi ya Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/23.

“Sekta binafsi ikinawiri na Serikali inanawiri! Kwa sababu sekta binafsi ndiyo injini ya kuwezesha ukuaji wa uchumi wetu, kwa hiyo niwashukuru kwa maoni mliyotoa yakiwemo ya kutoza kodi maeneo yenye kipato kikubwa na kutoa msamaha wa kodi kwa wale wenye kipato kidogo ili kupunguza pengo la walio nacho na wasio nacho”, alisema Dkt. Nchemba.

Aliwaelekeza wataalamu wa Wizara hiyo kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kupitia mapendekezo yaliyotolewa na wadau hao ili kuona namna bora ya kuyatumia mapendekezo hayo.

Aidha, Waziri Nchemba alitoa wito kwa wadau wengine ikiwemo Sekta binafsi nchini kuwasilisha mapendekezo na maoni yao mapema kuelekea maandalizi ya Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2022/2023 ili kuwa na sera za kikodi rafiki kwa ajili ya kuharakisha maendeleo ya nchi.

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Nnauye, alisema kuwa mawazo yaliyotolewa na wadau ni mazuri na kuwa Serikali imeyachukua na yatafanyiwa kazi na kuiomba Wizara ya Fedha kuchambua maoni hayo mapema na kuwashirikisha wadau kuhusu maamuzi yatakayofikiwa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Jamal Kassim Ali, alisema kuwa suala la kuangalia namna ya kuzitoza kodi kampuni kubwa duniani zinazofanya biashara kwa njia ya mtandao ni muhimu kwa kuwa yanakusanya fedha nyingi kutoka kwa wananchi lakini haziachi chochote kwa ajili ya maendeleo yao.

Chama cha Watoa Huduma za Simu Tanzania (TAMNOA) walisema kuwa mapendekezo waliyoyatoa yakifanyiwa kazi na kuanza utekelezaji wake mapato ya Serikali yataongezeka kutoka asilimia 61 hadi asilimia 64.9.

Mwigulu “Sekta binafsi ikinawiri na Serikali inanawiri“ Mwigulu “Sekta binafsi ikinawiri na Serikali inanawiri“ Reviewed by Cadotz media on 7:28 PM Rating: 5

No comments

Comment to Cadotz

Ndugu ahsante kwa kuitembelea Cadotz, Endelea kufurahia huduma zetu pia Tunakusogezea Cadotz uchague unachokitaka katika menyu zetu.
Bofya chini

<<< rudi